UPASUAJI wa kuzibua mishipa ya moyo bila kufungua kifua kwa kupitia 
mshipa wa damu wa mkono kwa wagonjwa 33 uliofanywa na madaktari wa 
Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) umeibua maajabu mapya kwa 
taasisi hiyo inayozidi kujipatia umaarufu mkubwa duniani.
Kwa mara ya kwanza tangu taasisi hiyo imeanza kutoa huduma ya 
matibabu ya upasuaji wa moyo bila ya kufungua kifua, hatimaye imeweza 
kufanya upasuaji huo wa kuzibua mishipa ya moyo kupitia mshipa wa damu 
wa mkono.
Awali wakati huduma hiyo iliponzishwa katika taasisi hiyo ya JKCI, 
upasuaji uliokuwa unafanywa kwa wagonjwa waliofika hospitalini hapo 
ulikuwa ni ule wa kutumia mishipa ya paja.
Hata hivyo katika tukio la hivi karibuni, madaktari bingwa wa JKCI 
kwa kushirikiana na wenzao wa Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya 
Misaada (IIRO) ya nchini Saudi Arabia walifanya upasuaji huo wa kuzibua 
mishipa ya moyo kupitia mshipa wa damu wa mkono kwa kutumia mtambo wa 
Cathlab kwa wagonjwa hao 33.
Upasuaji huo wa moyo uliofanyika katika kambi hiyo ya JKCI ambayo 
ilianza Novemba 15, mwaka huu hadi jana ni ya upasuaji wa bila kufungua 
kifua kwa watu wazima. Pamoja na kuwepo kwa faida mbalimbali kutokana na
 upasuaji huo, utafiti wa gazeti hili umebaini kutokea kwa maajabu 
mbalimbali kutokana na upasuaji huo.
Ajabu la kwanza la upasuaji huo ni ule ambao sasa utamwezesha mgonjwa
 kutoka chumba cha upasuaji akiwa anatembea tofauti na upasuaji wa awali
 ambapo mgonjwa hakuweza kutoka kwenye chumba cha upasuaji akiwa 
anatembea.
Hiyo ilitokana na upasuaji wa awali kufanyika kwa kutumia mishipa ya 
paja ambapo mgonjwa alikuwa analazimika kupasuliwa paja ili kupata 
mishipa yake iliyokuwa inatumika katika kufanya matibabu hayo ya moyo.
Ajabu la pili kutokana na upasuaji huo mpya na wa aina yake; ni lile 
la mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji huo wa kuzibua mishipa ya moyo bila 
kufungua kifua kuruhusiwa kurudi nyumbani baada ya saa nne tangu 
afanyiwe upasuaji.
Hatua hiyo ni tofauti na upasuaji wa awali wa kutumia mshipa wa paja 
ambapo mgonjwa alikuwa analazimika kukaa hospitali kwa zaidi ya saa 24 
ili kuangalia maendeleo ya afya yake.
Ajabu la tatu katika matibabu hayo ni hatua ya wageni hao kutoka 
Taasisi ya IIRO kujifunza vitu vingi na kupata uzoefu mpya wa baadhi ya 
magonjwa na mambo ya kiteknolojia katika Taasisi ya JKCI ambayo katika 
nchi yao hakuna.
Mufti awafumbua macho
Watanzania Akizungumzia matibabu hayo ya aina yake jana; Shehe Mkuu 
wa Tanzania; Mufti Abubakar Zubeir aliwaasa Watanzania kupata matibabu 
hasa ya magonjwa ya moyo hapa nchini ili kuepuka gharama za kwenda 
kupata matibabu nje ya nchi ambako gharama yake ni kubwa.
Shehe Zubeir alitoa mwito huo katika hafla ya kuwaaga madaktari hao 
bingwa wa IIRO wa Saudi Arabia waliofika nchini kushirikiana na wenzao 
wa JKCI katika upasuaji huo. “Kazi iliyofanywa hapa ni kuhakikisha watu 
wanapata tiba nzuri, watu wasiende nje ya nchi kutibiwa kwani gharama 
yake kwa mtu mmoja ni zaidi ya shilingi milioni 30, niwashitue 
Watanzania kuwa tiba hizi zinapatikana hapa kwenye taasisi hii ya JKCI,”
 alisema.
Alisema gharama ambayo mgonjwa atakwenda kutibiwa nje ya nchi ni 
kubwa ambapo si watu wengi wanaweza kuimudu ndiyo maana serikali pamoja 
na taasisi nyingine wameomba kambi hizo za matibabu kuja nchini kufanya 
matibabu na pia kutoa ujuzi wa madaktari waliopo.
Mkurugenzi JKCI ahimiza upimaji wa afya
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya JKCI, Profesa Mohamed Janabi
 alisema kambi hiyo ya madaktari kutoka Saudi Arabia ilienda sambamba na
 kutoa mafunzo kwa madaktari wa JKCI na pia kubadilishana ujuzi kitu 
ambacho kimewajengea uwezo.
“Faida ya upasuaji wa aina hii ni kumuwezesha mgonjwa kutoka chumba 
cha upasuaji akiwa anatembea mwenyewe na baada ya saa nane anaweza 
kuruhusiwa kutoka hospitali kama anaendelea vizuri, kwa hiyo kambi hii 
ni faida sana kwetu,” alisema Profesa Janabi.
Aidha aliwasisitiza wananchi kupima afya zao mara kwa mara jambo 
ambalo litawasaidia kujua kama wana matatizo ya moyo hivyo kupata tiba 
kwa wakati. “Changamoto kubwa tunayokutana nayo ni kuwa wagonjwa wengi 
tunaowapokea ni mioyo yao kuwa katika hali mbaya.”
Aliishukuru taasisi ya IIRO kwa kutuma wataalamu hao kuja kutoa 
huduma ya matibabu ambayo iliambatana na mafunzo kwa madaktari wa 
taasisi ya JKCI.
Balozi, Wizara wasifu ushirikiano
Balozi wa Saudi Arabia nchini, Mohammed bin Mansour Almalik alisema 
kuja kwa madaktari hao ni ishara kwamba Tanzania na Saudi Arabia wana 
ushirikiano mzuri, alisema ushirikiano huo hautaishia kwenye sekta ya 
afya pekee bali pia katika sekta nyingine.
Mwakilishi wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na 
Watoto, Dk Dorothy Gwajima alisema wizara hiyo itaendeleza ushirikiano 
wa aina hiyo na taasisi mbalimbali ili wataalamu wa ndani katika sekta 
ya afya wapate ujuzi wa kutosha na pia kujifunza teknolojia mpya kuepuka
 gharama za kumpeleka mgonjwa kutibiwa nje ya nchi.
 
 
 
 Hello, my name is Jack Sparrow. I'm a 50 year old self-employed Pirate from the Caribbean.
Hello, my name is Jack Sparrow. I'm a 50 year old self-employed Pirate from the Caribbean. 
No comments:
Post a Comment